Jumapili, 30 Juni 2013

UHIFADHI WA MBEGU KWA AJILI YA MZUNGOKO MWINGINE WA UPANDAJI SAMAKI BWAWANI NA MATATIZO KATIKA UFUGAJI SAMAKI..


Unapovuna samaki, hakikisha kuwa vifaranga au samaki wazazi utakaokuwa umewachagua wanawekwa katika kijibwawa kingine (kinachojulikana kama nursery pond) kabla ya kuwarudisha bwawa la kukuzia (production pond). Ni muhimu kufanyia bwawa matengenezo na kulijaza maji kabla ya kuweka samaki tena. Hili ni muhimu kwa mfugaji kwani kinamhakikishia mfugaji kujua kuwa anapanda mbegu changa na ambao  hawajadumaa. Pia humhakikishia kujua kuwa samaki waliopandwa wanalingana na ujazo wa bwawa, yaani vifaranga viwili kwa kila mita moja ya mraba na pia hurahisisha maji ya bwawa kurutubika kirahisi.

MATATIZO YA UFUGAJI SAMAKI
Ingawa ufugaji wa samaki si kazi ngumu sana, kuna matatizo mbali mbali ambayo mfugaji anaweza 
kukumbana nayo. Lakini, matatizo mengi yanaweza kuepukika kama mfugaji ataweza kufuata kikamilifu 
maelekezo ya ujengaji na utunzaji wa bwawa.
  1. Tatizo mojawapo ni la kuvuja kwa kuta za bwawa. Tatizo hili hutokea iwapo ujengaji wa bwawa haukufuata maagizo na taratibu za ujengaji wa bwawa. Iwapo utakumbana na tatizo hili, muone afisa uvuvi aliye karibu nawe upate ushauri.
  2. Tatizo la maadui wa samaki kama vile ndege, kenge, fisi maji, nyoka hutokea. Kwa kiasi kikubwa tatizo hili huambatana na ujengaji bwawa mbali na nyumbani na bwawa kuwa na nyasi nyingi (halifyekewi). Suluhisho ni kufweka nyasi kila mara, kujenga uzio kwa kutumia matete na hata nyaya za seny’enge, kuwinda ndege na kuharibu mazalia/maskani yao, bwawa kuwa karibu na maskani ya watu.
  3. Kudumaa kwa samaki kutokana na kuwa wengi bwawani kupita idadi inayotakiwa. Tatizo hili hutokana na kutokukaushwa bwawa kwa kipindi kirefu. Utatuzi huweza kuwa; kukausha bwawa kila baada ya miezi 6 hadi 9
  4. Ugumu wa kukausha maji bwawani. Husababishwa na bwawa kujenjwa kwenye eneo la tambarare kiasi kuwa hakuna uwezekano wa kutumia bomba au kukata kuta za bwawa kuondoa maji. Utatuzi; chimba bwawa kwenye eneo lenye mteremko wa wastani
  5. Bwawa lisilo kaushika huwa mazalia ya Mbu wakati linapokuwa halina samaki ndani yake na kusaidia kuenea kwa malaria. Konokono wenye mabuu ya kichocho huzaliana kwenye mabwawa yenye kina kifupi au yenye majani mengi. Ni vema kuwa na bwawa yenye kina cha kutosha, lisilo na nyasi au majani ndani yake na linaloweza kukaushika kirahisi ili kuondokana na matatizo haya.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni