Jumapili, 30 Juni 2013

URUTUBISHAJI WA BWAWA LA SAMAKI KWA MBOLEA NA (MAJIVU) PAMOJA NA USAFIRISHAJI WA VIFARANGA WA SAMAKI.


  1. Kutegemea aina ya udongo, majivu ya moto huweza kutawanywa bwawani kabla ya kuingiza maji ili kupunguza Tindikali ya udongo na kuua baadhi ya wadudu walio maadui wa samaki waliopo katika eneo la bwawa.
  2. Mbolea huweza kutawanywa bwawani kabla ya kuweka maji ili kusaidia kujenga mazingira ya maji kutuama (yaani Kushikamanisha udongo).
  3. Vinginevyo, mbolea huwekwa eneo maalum (Uzio) mara baada ya maji kuingizwa bwawani ili kulirutubisha na Kuliwezesha liwe na vijimea na vijidudu vidogo vidogo vitakavyokuwa chakula cha awali cha samaki.
  4. Dalili za kuwepo kwa vijimelea hivyo bwawani ni kugeuka rangi ya maji na kuwa ya kijani.
  5. Aina ya mbolea hutegemea upatikanaji wake. Samadi ya ng’ombe, mbuzi, kondoo, nguruwe, kuku, bata na hata Majani mabichi yaozayo kirahisi na yasiyo sumu kwa wanyama na binadamu huweza kutumika.
  6. Kiasi cha kuweka mbolea hutegemea sana ukubwa wa bwawa, aina ya samadi na idadi ya samaki waliomo.
  7. Kipimo kizuri cha kiasi kinachotosha ni kuingiza mkono ndani ya maji hadi kufikia kwenye kiwiko, na usipoona Kiganja chako, basi simamisha uwekaji wa mbolea kwani vijimelea na vijidudu waliomo wanatosha kulisha samaki Waliomo kwenye bwawa kwa muda wa siku kadhaa.
  8. Ukizidisha mbolea ni hatari kwa samaki, kwani wanaweza kufa kwa kukosa hewa ya oksijeni, hasa nyakati za usiku.



Usafirishaji, upandaji na ulishaji wa vifaranga wa samaki

USAFIRISHAJI WA VIFARANGA WA SAMAKI
Upatapo vifaranga, visafirishe wakati wa asubuhi kwa kutumia ndoo ya plastiki, chungu, maplastiki makubwa.

Weka kiasi cha vifaranga 200 katika ndoo moja. Ni vema mkulima kuwa na tabia ya kupunguza maji 
kwenye ndoo yenye samaki na kuweka mengine afikapo eneo lenye maji.

Ufikapo bwawani, inamisha ndoo ili maji ya kwenye ndoo yaingiliane na yale ya bwawani. 
Hii ni kuruhusu joto la maji na mazingira ya maji yaingiliane na kuwa sawa.

Waruhusu samaki watoke bwawani wenyewe bila ya kuwamwaga. Itachukuwa muda kabla ya vifaranga wote kuingia bwawani. Kwa kufanya hivyo, samaki hawatapata mshituko ambao wanaweza kupata kama 
watamwagwa. Mshituko wa   ghafla huweza kusababisha vifo.


UPANDAJI WA VIFARANGA VYA SAMAKI.
Ubora wa samaki utakao wafuga utategemea sana ubora wa vifaranga utakaokuwa umepanda bwawani.

Chanzo chako cha vifaranga ni bora kiwe na vifaranga wenye umri mdogo na ambao hawajadumaa.

Kwa samaki aina ya Perege, panda vifaranga viwili (2) hadi watatu (3) kwa kila mita moja ya mraba.

Kwa sasa,  samaki aina ya Perege ndio wanaoshauriwa kufugwa na wafugaji wa maji baridi hapa nchini.

Kambale huweza kufugwa na mkulima mzoefu kwani huduma yake huitaji mtaji mkubwa katika 
kuwalisha na Utaalam katika kuzalisha vifaranga vyake.


ULISHAJI WA SAMAKI.

  1. Samaki, Kama walivyo wanyama wengine, wanahitaji kula.
  2. Chakula cha samaki huweza kugawanywa katika makundi mawili:-
  3. Cha asili kipatikanacho ndani ya bwawa kama vile vijimea, vijidudu na samaki wadogo.
  4. Cha ziada ambacho huongezwa bwawani na mkulima.
  5. Ili chakula cha asili kipatikane bwawani, ni vema bwawa liwe limerutubishwa vizuri, kwani vijimea vinavyotarajiwa humea palipo na rutuba.
  6. Chakula za ziada huwekwa bwawani na mkulima mwenyewe. Aina ya chakula cha ziada hutegemea upatikanaji wake, gharama na aina na ukubwa wa samaki. Baadhi ya chakula cha ziada ni kama: pumba za mahindi, za mpunga, mashudu ya pamba na karanga, machicha ya pombe, ugali na masazo ya jikoni, baadhi ya majani pori, majani yatokayo bustanini.
  7. Inashauriwa mfugaji alishe kila siku, kwa muda ule ule, saa ile ile na sehemu ile ile. Tabia hii hujenga mazoea ya samaki kula zaidi na kupunguza wingi wa chakula kinachopotea.
  8. Usilishe chakula kingi zaidi ya mahitaji ya samaki kwa siku hiyo. Mfano, usiweke debe zima la pumba kwa mara   moja na kuacha kulisha kwa wiki nzima! Sehemu ya chakula kitakachosalia, kitaoza na baadhi ya siku samaki hawatakuwa na chakula, watashinda na kulala njaa!




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni